Huyu ndiye dada aliyefunika ufaulu Chuo Kikuu Dar

Ni binti,apiga A=32,B+=6 katika masomo 38, Amesoma shule za kawaida za serikali

 Mhitimu bora wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwaka 2014, Doreen Kabuche (22), aliushangaza umma uliohudhuria maafali ya 44 ya chuo hicho baada ya kutangazwa kuwa kinara kwa ufaulu kwa kupata alama A 32 na B+ sita kati ya masomo 38 ya shahada ya Takwimu Bima (Actuarial Science).

Kwa alama hizo, Doreen alipata wastani wa alama za ufaulu (GPA) 4.8 na kuacha alama ya 0.2 ili kufikia kiwango cha juu kabisa cha ufaulu cha alama tano, hivyo kupata shahada ya kwanza daraja la kwanza.

Akizungumza na NIPASHE katika mahojiano maalum mwishoni mwa wiki, Doreen anayeishi Kigogo Mwisho, jijini Dar es Salaam alihitimu shahada hiyo akiwa miongoni mwa wanafunzi 28 wa darasa lake, lakini akihitimu sambamba na wanafunzi wengine 5,745, wanawake wakiwa ni 2,298 wa shahada ya kwanza.

Shahada hiyo inayotolewa katika Shule ya Sayansi ya Asili (CoNaS) chuoni hapo, ni miongoni mwa taaluma adimu nchini. Ilianza kufundishwa chuoni hapo mwaka 2011.
Miongoni mwa taasisi ambazo zitafurahia taaluma hiyo kuanza kupata wataalam nchini ni pamoja na mifuko ya hifadhi ya jamii ambayo hulipa fedha nyingi kupata huduma hiyo kwa wataalam kutoka nje ya nchi na kwa gharama kubwa.

Alipopewa nafasi ya kuzungumza mbele ya mamia ya wanafunzi wenzake na wageni waalikwa kwenye ukumbi wa Mlimani City, aliishia kutoa shukrani kwa wahadhiri, wanafunzi wenzake na wote waliomsaidia katika mafanikio yake kitaaluma.

Ili kupata wastani wa ufaulu wa daraja la kwanza kwa kiwango cha GPA ya 4.8, mhitimu hulazimika kufaulu kwa kiwango cha juu kwa miaka yote ya kuwa chuoni. Doreen alifanikiwa kutimiza sharti hilo baada ya kufaulu masomo 32 kwa kiwango cha ‘A’ na masomo mengine sita kufaulu kwa alama za B+ kati ya masomo yote 38 ya shahada yake; baadhi ya yale yaliyomkwamisha kupata A yakiwa ni ‘Actuarial Mathematics’ na ‘Legal Matters in Actuarial Industry’.

Mgawanyo wa ufaulu wake kwa mwaka wa kwanza ulikuwa ni A za masomo 12 na B+ za masomo mawili kati ya masomo 14; mwaka wa pili alifaulu kwa kupata A katika masomo 10 na B+ mbili kati ya masomo 12 na mwaka wa tatu alifaulu pia kwa kiwango cha alama A katika masomo 10 na masomo mengine mawili akapata B+ kati ya masomo 12.

ALIKOTOKA
Tofauti na fikra za wengi kuwa siku hizi wanafunzi bora hutoka katika shule zinazotoza ada kubwa na kutumia Kiingereza kama lugha kuu ya mawasiliano, maarufu kama English medium’, Doreen anathibitisha kuwa hilo halina ukweli.

Katika mahojiano na NIPASHE, alisema kuwa hajawahi kusoma katika shule hizo zinazotoza ada kubwa za mamilioni ya fedha na badala yake, alipitia katika shule za serikali kuanzia shule ya msingi mwaka 2004 hadi kidato cha sita mwaka 2011.

“Shule nilizosoma kabla ya chuo kikuu ni Mlimani (Shule ya Msingi) iliyopo Chuo Kikuu Dar es Salaam sehemu ya Mlimani, kidato cha kwanza hadi cha nne nilimaliza katika sekondari ya Forodhani na kidato cha tano na sita katika shule ya sekondari Benjamin Mkapa. Kote huko usafiri wangu siku zote ni wa daladala.

“Na kama unavyojua, ni kugombana na makondakta kila asubuhi wakati wa kupanda mabasi (daladala) kwenda shule na jioni wakati wa kurudi. Ila yote hayo tumeyazoea na hivyo adha za usafiri hazikuwa tatizo kubwa,” alisema Doreen na kuongeza:

“Juhudi, kujiamini na kuzingatia maelekezo ya walimu ni muhimu. Aina ya shule ni nyongeza tu kwa sababu siyo wote wanaosoma shule hizo za kitajiri wamekuwa wakifaulu. Wapo wanaofanya vizuri, na wapo wanaofeli pia... ni kama ilivyo kwenye hizi shule zetu (shule za serikali).”

KINARA KIDATO CHA SITA
Mafanikio ya sasa ya Doreen hayakuja kwa bahati mbaya. Historia yake inaonyesha kuwa kila hatua aliyopita alikuwa akifanya vizuri. Katika matokeo yake ya kidato cha nne mwaka 2008, Doreen alifaulu kwa kiwango cha daraja la kwanza akipata pointi tisa na kuchaguliwa kuendelea kidato cha tano katika Shule ya Sekondari Benjamin William Mkapa baada ya kuchagua mchepuo wa Uchumi, Hisabati na Jiografia (EGM).

Doreen aliendeleza makali yake katika mitihani yake ya kidato cha sita baada ya kufaulu kwa kiwango cha daraja la kwanza kwa pointi nne na kuwa kinara wa mchepuo wa EGM Tanzania.

Kwa matokeo hayo, akapata nafasi ya kuwa miongoni mwa wanafunzi bora Tanzania walioitwa bungeni mwaka 2011 na kutambulishwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, mbele ya wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kushangiliwa na wote waliokuwamo ukumbini.

“Hapo shauku yangu ya kutaka kuongeza juhudi zaidi na kufanikiwa kama akina Migiro (Asha-Rose), akina Tibaijuka (Profesa Anna) na akina Spika Anne Makinda ikaongezeka. Nikapania kufanya vizuri hadi chuoni na sasa namshukuru Mungu kuwa hatua hiyo pia nimeivuka salama na kufanikiwa,” alisema Doreen.

Pamoja na mafanikio yake kuanzia kidato cha kwanza hadi cha sita, Doreen alisema kuwa hajawahi kujihusisha sana na masomo ya ziada maarufu kwa jina la tuition na badala yake, alitumia muda mwingi kujisomea, kujadiliana na wanafunzi wenzake na mara kadhaa kusaidiwa masomo nyumbani na mjomba wake Charles Mayalla wa Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT).

Doreen alitangazwa kuongoza kwa ufaulu Chuo Kikuu Dar es Salaam ikiwa ni siku chache tu baada ya msichana mwingine aitwaye Rachel Kiunsi wa Shule ya Msingi Kimara 'B' jijini Dar es Salaam kuwa kinara wa somo la Hisabati Tanzania baada ya kupata alama zote za somo hilo katika mithani ya taifa ya darasa la saba.

MATARAJIO
Baada ya kumaliza shahada ya kwanza, matarajio ya sasa ya Doreen ni kuendelea na masomo ya shahada ya uzamili (masters) ambayo hata hivyo, anasema mchakato wake (kwa masomo ya Actuarial Science) ni ghali kwani kabla ya kujiunga anatakiwa kufanya mitihani kadhaa kabla ya kuanza shahada hiyo.

“Gharama za mithani hii ni kubwa. Kuna mitihani ya hatua nyingi hadi kupata nafasi ya kuanza kusomea masters na gharama zake kwa ujumla hufikia hadi Sh. milioni 10. Hizi ni gharama kubwa. Ila kwa sasa sijakaa bure.

Wazazi wangu bado wananiunga mkono na mwenyewe pia nimejifunza kuwa mpambanaji tangu wakati nikigombana na makonda ili kupanda daladala na kuwahi shule,” alisema Doreen.

“Na hata sasa nimeshaanza mapambano ili kujiendeleza zaidi. Nimepata kazi na fedha ninazopata nitaendelea kuzidunduliza kila mwezi ili nitimize ndoto zangu. Hata kama nitalazimika kusubiri kwa mwaka na zaidi, nitasubiri na mwishowe naamini kuwa Mungu ataniwezesha na kufanikisha malengo,” alisema Doreen.

“Najua hata hawa kina (Prof.) Tibaijuka, Migiro na wengine hawakufika walipo sasa kirahisi. Walipambana, na mimi pia ninapambana ili siku moja kufikia level zao,” alisema Doreen.

WAZAZI, FAMILIA
Akiwaelezea wazazi wake, Doreen alisema kuwa baba yake (Kabuche) aliwahi kuwa mfanyakazi wa benki kabla ya kuacha na kuwa mjasiriamali ambaye hivi sasa yuko Mtwara. Mama yake aitwaye Janeth Kabuche pia ni mjasiriamali.

Doreen alisema anawashukuru sana wazazi wake kwani mara zote wamekuwa wakimsaidia kwa kila hali ili kutimiza malengo yake katika elimu.  Alisimulia kuwa hata alipotia fora kwa kutwaa zawadi za masomo yote wakati wa mahafali ya kidato cha sita shuleni kwao Benjamin Mkapa mwaka 2011, wazazi wake walimtia moyo kwa kumnunulia kompyuta mpakato (laptop) aina ya Dell.

“Kwetu nimezaliwa peke yangu. Nikishatulia na kuanza maisha yangu binafsi baada ya kumaliza mambo ya masomo nitapenda kuwa na watoto wengi ili kuongeza ukubwa wa familia... walau wafikie watoto saba hivi.”

DINI, MUZIKI, FILAMU
Licha ya kufanya vizuri katika masomo, Doreen huwa haachi kujihusisha na masuala mengine ya kijamii.

“Kila Jumapili huwa sikosi kwenda kwenye ibada katika kanisa letu la Kigogo Luhanga. Vilevile mimi ni mpenzi wa muziki kama wa bendi ya Wazee wa Ngwasuma (FM Academia), bongofleva na filamu pia huwa ninazitama... (filamu) ninayoipenda inaitwa Think Like a Man, Act Like a Woman,” alisema Doreen.

RATIBA AKIWA CHUONI
Doreen alisema kuwa wakati wote akiwa chuoni alizingatia ratiba kuu aliyojiwekea kila uchao, ambayo ni kwenda darasani bila kukosa kipindi chochote na baada ya hapo alikuwa hakosi majadiliano na wanafunzi wenzake kama Catherine John na Shamim Nuah.

“Sikuwahi ku-dodge (kukacha) kipindi, sikuwahi pia kukosa discussion na wenzangu bila sababu ya maana. Na siku moja moja za mwisho wa wiki tulikuwa tukienda ku-refresh mind na wenzangu, hasa maeneo ya viwanja vya Sinza na siku nyingine Mlimani City. Ila kila Jumapili ni lazima kwenda kanisani pale chuo au kanisa la nyumbani kwetu Kigogo Luhanga,” alisema Doreen.

Doreen ana ndoto za akufuata nyayo za kina  Prof. Anna Tibaijuka, Dk. Asha-Rose Migiro na Anne Makinda kwa kuwa ni miongoni mwa wanawake waliofanikiwa katika medani za taaluma, uongozi na siasa.

Post a Comment

Previous Post Next Post