Asha-Rose Migiro ni moja kati ya waliochukua fomu ya kuomba ridhaa ya Chama cha Mapinduzi ya kupitishwa kugombea nafasi ya Urais katika uchaguzi mkuu mwezi oktoba kupitia tiketi ya chama hicho. Migiro ni miongoni mwa waliotajwa tano bora za urais CCM Ingawa hakuwa akitajwa mara kwa mara kwamba ni mmoja wa wagombea tishio, kupitishwa kwa jina la Dk Asha-Rose Migiro kuingia katika tano bora ya kuwania urais kwa tiketi ya CCM, siyo jambo la ajabu. Rekodi yake kitaifa na kimataifa lakini pia jinsia, ni mambo ambayo yamechangia kwa kiasi kikubwa Waziri huyo wa Katiba na Sheria, kuvuka hatua hiyo ya kwanza. Dk Migiro ambaye pia ni Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa, Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa ya CCM, alijitosa katika safari ya kuelekea Ikulu Juni 15 pasi na mbwembwe za aina yoyote. Mtanzania huyo ambaye aliweka rekodi ya kuwa Mwafrika wa kwanza mwanamke kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), alikuwa akitajwa kuwa anaweza kuwa mwanamke wa kwanza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano. Hakuwahi kutangaza nia kama ilivyokuwa kwa makada wengine waliotumia fursa hiyo kuelezea mikakati yao lakini pia, hakuwa na mbwembwe katika kutimiza sharti la kusaka wadhamini mambo ambayo pengine yalimwongezea sifa za kupitishwa miongoni mwa wagombea 38 waliokuwa wamechukua na kurejesha fomu kuomba nafasi hiyo ya juu kabisa katika utawala wa nchi. Lakini kigezo kingine kilichomvusha ni umakini wake na kutokulengwa na mishale ya kashfa ambazo ziliwakumba mawaziri kadhaa katika Serikali ya Awamu ya Tano na yote hayo yanampa fursa kubwa ya kufika mbali katika safari yake hiyo hasa ikiwa hoja ya nafasi ya wanawake kushika urais kama ilivyokuwa katika uchaguzi wa Spika wa Bunge la 10 itatiliwa maanani. Dk Migiro alianza kutajwatajwa miongoni mwa wanaoweza kumrithi Rais Jakaya Kikwete baada ya kumaliza mkataba wake Umoja wa Mataifa na kurejea nchini na mara moja kuteuliwa kuwa mbunge na Waziri wa Katiba na Sheria. Msimamo wake Wakati akizunguka katika mikoa mbalimbali kusaka saini za wadhamini, Dk Migiro alikuwa makini katika kuzungumza huku akisisitiza kuwa anasubiri Ilani ya CCM... “Na mimi nitaweka mikakati ya kuendeleza yale ambayo yameshafanyika. Sasa endapo nitapata ridhaa ya chama changu, nyenzo yangu kuu itakuwa ni Ilani ya Uchaguzi ya CCM.” Alisema kwa kuwa uchumi umeendelea kukua awamu hadi awamu, naye atahakikisha kukua huko kunawafikia wananchi wengi zaidi: “Nitahakikisha kuwa mambo haya yaliyofanywa na awamu za uongozi zilizopita yanakuwa stahamilivu na endelevu na kuwafikia wananchi walio wengi zaidi.” January Makamba ni moja kati ya waliochukua fomu ya kuomba ridhaa ya Chama cha Mapinduzi ya kupitishwa kugombea nafasi ya Urais katika uchaguzi mkuu mwezi oktoba kupitia tiketi ya chama hicho. January ni miongoni mwa waliotajwa tano bora za urais CCM Alijiandaa na haikushangaza kusikia akiwa miongoni mwa wagombea watano waliovuka katika mchujo wa Kamati Kuu (CC) na kuingia katika hatua ya kupigiwa kura na Halmashauri Kuu (NEC). Tangu alipotangaza nia, January Makamba (41), amekuwa katika hekaheka za kujitangaza na kujinadi siyo kwa wanaCCM pekee, bali hata wananchi kupitia machapisho mbalimbali. Hata hivyo, hadi mwaka 2012, Naibu Waziri huyo wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, hakuwa na mipango ya kugombea urais. Aliwahi kuhojiwa katika kipindi cha mikasi cha Televisheni ya EATV na kusema hana mpango huo kabisa. Pengine Mbunge huyo wa Bumbuli alikuwa na lake moyoni kwani Julai 2, mwaka jana aliweka bayana nia yake wakati alipohojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya BBC na kusema atagombea urais kwa sababu Tanzania inamhitaji mtu mwenye sifa kama zake, wa kizazi cha sasa. Tangu wakati huo, January amefanya mambo mengi ya kujizatiti kwenye nia yake hiyo ikiwamo kutoa kitabu maalumu cha maswali 40, kilichoandikwa na mwandishi Privatus Karugendo kikionyesha kikijibu maswali mbalimbali kuhusu namna mwanasiasa huyo kijana atakavyoweza kupambana na changamoto za urais iwapo chama chake kitampa ridhaa na Watanzania wakamchagua. Wakati akiendelea na harakati zake Februari, 2014 yaliibuka mambo yasiyotarajiwa baada ya vikao vya CCM kutoa “onyo” dhidi yake na wanachama wengine watano kuwataka wasiendelee na “mchezo mchafu” wa kampeni za urais kabla chama hicho hakijaanzisha mchakato huo rasmi, hapo ndipo wengi wakang’amua kwamba January anausaka urais wala hatanii. Mtoto huyo wa Katibu Mkuu mstaafu wa CCM, Mzee Yusuph Makamba, aliingia rasmi kwenye siasa mwaka 2010 alipoomba ridhaa ya CCM kuwa Mbunge wa Bumbuli, wilayani Lushoto na katika kura za maoni za chama hicho, alimshinda mbunge mzoefu, William Shelukindo kwa kupata kura 14,612 dhidi ya 1,700. Baada ya kushinda ndani ya chama chake, January hakukutana na mpinzani yeyote kwenye Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 na hivyo akaingia kwenye rekodi ya wabunge waliopita bila kupingwa. Katika Bunge la 10, alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini na mwaka 2011, CCM ilimteua kuwa Katibu wa Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa akichukua nafasi ya Benard Membe. Alitumikia wadhifa huo ndani ya chama chake hadi mwaka 2012 alipomuachia Dk Asha-Rose Migiro. Katika Mkutano Mkuu wa Nane wa CCM, January alichaguliwa kuwa kati ya wajumbe 10 wa Kamati Kuu ya chama kutoka upande wa Tanzania Bara akipata kura 2,093. Atangaza nia mara ya pili Juni 7, akiwa Dar es Salaam, January alitangaza nia kwa mara nyingine ya kuwania urais akiahidi kwamba Serikali yake itaunda baraza la mawaziri wasiozidi 18 wasiotiliwa shaka na wananchi juu ya uwezo na uadilifu wao. John Pombe Magufuli ni moja kati ya waliochukua fomu ya kuomba ridhaa ya Chama cha Mapinduzi ya kupitishwa kugombea nafasi ya Urais katika uchaguzi mkuu mwezi oktoba kupitia tiketi ya chama hicho. Magufuli ni miongoni mwa waliotajwa tano bora za urais CCM Dar es Salaam. Kama alivyowashangaza wengi pale alipojitokeza kuchukua fomu za kuomba kuteuliwa na CCM kuwania urais Mei 29 mwaka huu, ndivyo Dk John Magufuli alivyowashangaza tena jana kufikia hatua hii ya tano bora. Bila makeke, majivuno wala majigambo, Magufuli ambaye ni waziri wa ujenzi alipochukua fomu alisema tu kuwa kipaumbelea chake ni kutekeleza ilani ya uchagzi ya CCM. Hata katika safari yake ya kusaka wadhamini mikoani, mbunge huyo wa Chato alikwenda kimya kimya, bila mbwembwe, ahadi wala kukusanya mashabiki. Bila hiyo ndiyo siri yake ya ushindi, alihofia kukatwa mapema kwa kukiuka masharti ya chama, kama ilivyowatokea wengine. Hata kabla hajachukua fomu, Dk Magufuli hakuwahi kutangaza nia yake ya kuwania urais, hadi alipoibuka ghafla na papo hapo akapenya hadi hatua hii muhimu, hadi alipolidokeza gazeti hili mjini Dodoma. “Swali hili nimeulizwa mara nyingi. Mara zote nimekataa kulijibu kwa sababu katika chama chetu (CCM) kuna utaratibu wake wa namna ya kuomba nafasi ya uongozi. Muda ulikuwa haujawadia. “Lakini utakumbuka wiki hii hapa hapa Dodoma, vikao vya juu vya chama chetu vimetoa ratiba kwa wanaotaka kuwania nafasi mbalimbali kujitokeza. Kwa maana hiyo sasa niko huru kujibu swali lako kwa kusema rasmi ‘nitagombea urais’. “Nafanya hivyo kwa sababu naamini ninazo sifa za kuchagua na kuchaguliwa kama mwanachama wa CCM kwa nafasi yoyote inayojitokeza kulingana na Katiba ya chama chetu na pia Katiba ya nchi,” alisema Dk Magufuli. Pamoja na kutokuwa na papara za kutangaza nia wala kuanza kupitapita kwa wanachama kutafuta kuungwa mkono, Dk Magufuli alikuwa vinywani mwa watu wengi, ndani na nje ya CCM, wakisema akiteuliwa anaweza kuleta ushindani dhidi ya upinzani. Waziri huyo wa muda mrefu na maarufu kwa kumbukumbu na kukariri takwimu mbalimbali, kila wizara anayokwenda inageuka maarufu na kuanza kusikika, lakini kazi kubwa inayomweka kwenye mwanga wa kisiasa nap engine hata kumfikisha katika hatua hii ni wizara ya Ujenzi na hasa usimamizi wa ujenzi wa miundombinu. Dk Magufuli alizaliwa katika Kijiji cha Rubambangwe kilichopo Wilaya ya Chato mkoani Geita, ndipo unapoweza kukutana na wananchi ambao wanafahamu maisha yake ya ujana na hatua alizopita hadi hadi hatua ya leo. Kuna simulizi za kusisimua kuhusu maisha ya Magufuli ambaye wananchi wengi wa jimbo lake wanamtumia kama alama ya ushindi, akihusishwa na mafanikio ya kujitenga kutoka Wilaya ya Biharamulo hadi wakapata jimbo na hatimaye Wilaya. Balozi Amina Salum Ali ni moja kati ya waliochukua fomu ya kuomba ridhaa ya Chama cha Mapinduzi ya kupitishwa kugombea nafasi ya Urais katika uchaguzi mkuu mwezi oktoba kupitia tiketi ya chama hicho. Amina Salum Ali ni miongoni mwa waliotajwa tano bora za urais CCM Mwanadiplomasia Amina Salum Ali alitangaza nia ya kuwania urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mei 21 jijini Dar es Salaam. Akizungumza kuhusu nia yake hiyo, Balozi Amina ambaye alikuwa Balozi wa Kudumu wa Umoja wa Afrika (AU) kwenye Umoja wa Mataifa (UN) alisema wanawake wamekuwa wanyonge kugombea nafasi za juu za uongozi kwa kukosa fedha, lakini sasa ni wakati mwafaka kwao kujiamini katika jamii wakiamini uongozi siyo fedha, bali ni uzalendo, kujikubali na kujiamini. “Nimeona nina uzalendo, ninajiamini na ninaweza kuifikisha nchi yangu katika uchumi mkubwa kwa kutumia rasilimali zilizopo, zikiwamo gesi, mafuta, kilimo na utalii. Ninajiamini kwamba wakati wangu umefika kuwaongoza Watanzania kwa kushika nafasi za juu,”alisema. Balozi Amina ambaye aliwahi kushika nafasi za juu za uongozi Serikali ya Zanzibar na ile ya Muungano, ukiwamo uwaziri wa fedha, alisema Serikali inatambua mchango wa wanawake katika jamii, hivyo kupewa nafasi kubwa kama vile ujaji na uhakimu ni kusaidia kuongeza ufanisi wao kiutendaji. “Wanawake wengi wanaogopa kujitokeza wakihofia kugombea nafasi za juu za uongozi kwamba kunahitaji fedha, hivyo wanaishia kuwa wanyonge. Siyo kweli, wajitokeze kwa wingi ili watimize ndoto za kuwajibika kwa Taifa lao,” alisema. Alisema sheria hazitoshelezi kumlinda mwanamke, lakini mfumo dume umepungua kwa kiasi kikubwa hata kama haijafikia asilimia 50 kwa 50, jambo analosema lazima liangaliwe kwa mtazamo mpya. Elimu yake Balozi Amina alihitimu Chuo Kikuu cha New Delhi , India - Shahada ya Uchumi (B.A), mwaka 1979, pia alisomea masuala ya utawala wa fedha na utafiti wa uendeshaji kwenye Taasisi ya Uongozi (Institute of Management) Pune, India mwaka 1980, pia mwaka 1981 alihitimu Chuo Kikuu cha Pune, India - (Symbiosis College of Management) -MBA in Marketing (Masoko) na mwaka 1983 Chuo Kikuu cha Helsinki, Finland - Diploma ya utafiti wa masoko na uuzaji wa bidhaa nje (mafunzo maalum ya PRODEC). Nyadhifa alizoshika Mwaka 1981 hadi 1982, Mchumi Mwandamizi -Tume ya Mipango Zanzibar, mwaka 1982 hadi 1983, Mkurugenzi Biashara za Nje - Wizara ya Biashara ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na mwaka 1983 hadi 984, Katibu Bodi ya Biashara Zanzibar- Wizara ya Biashara Zanzibar. Nafasi nyingine ni, mwaka 1984 hadi 1985, Mchumi Mwandamizi - Tume ya Mipango, Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Zanzibar, mwaka 1985 hadi 1990- Mbunge Bunge la Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, mwaka 1985 hadi 1986- Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mwaka 1986 hadi 1989- Waziri wa Nchi ,Wizara ya Mambo ya Nje.