Dk John Magufuli jinsi alivyoshambulia jukwaa Morogoro

 MGOMBEA Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk John Magufuli, amesema Serikali atakayoiongoza itajenga viwanda vikubwa, vya kati na vidogo ili kuongeza ajira na mapato ya Serikali, huku akiwaahidi wakazi wa Morogoro kufufua viwanda vyao.
Amesema hayo katika Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro katika moja ya mikutano mikubwa ya kampeni za uchaguzi, uliorushwa moja kwa moja na televisheni mbalimbali nchini.
Akizungumza katika mkutano huo, Dk Magufuli alisema mbali na kujenga viwanda, pia Serikali hiyo itatoa Sh milioni 50 kwa kila mtaa na kijiji kwa ajili ya wanawake na vijana kukuza mitaji yao ya biashara na kuanzisha biashara mpya, huku akiwahakikishia kutobughudhiwa.
Kuhusu elimu na afya, Dk Magufuli alisema kuanzia mwakani wanafunzi kutoka darasa la awali mpaka kidato cha nne, hawatalipa ada ya shule kwa kuwa Serikali atakayoiongoza itatoa huduma hiyo bure. Pia, alisema atashusha bei ya vifaa vya ujenzi ili wananchi wanaofanya kazi na biashara na kujipatia kipato halali, wajenge nyumba kwa gharama nafuu.
Kabla ya Dk Magufuli kuhutubia, Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete alipanda jukwaani na kusema akistaafu kwa kumkabidhi nchi Dk Magufuli, atalala usingizi.
Rais Kikwete alisema hakwenda mkoani huko kuhudhuria mikutano ya Dk Magufuli, bali alikwenda kuhudhuria kikao cha mkakati cha Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), kilichofanyika mkoani humo.
Kwa mujibu wa Rais Kikwete, kwa kuwa mgombea huyo alikuwa na ratiba ya kuhutubia mkutano katika uwanja huo, akaona ni vyema na yeye ahudhurie mkutano huo.
Alipopewa nafasi ya kumkaribisha mgombea huyo, Rais Kikwete alitumia fursa hiyo kuzungumza kidogo kilichofanyika Dodoma, wakati wa mchakato wa kumpata mgombea urais wa chama hicho.
Alisema walitumia muda mrefu kujadili kila mgombea kati ya wagombea 38 waliojitokeza kuwania nafasi hiyo, mpaka wakapata wagombea watano akiwemo Dk Magufuli, Balozi Amina Salum Ali, Dk Asha-Rose Migiro, Bernard Membe na January Makamba.
Baada ya hapo, alisema walikwenda katika kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM ambako wafuasi wa mmoja wa wagombea ambaye hakuingia katika tano bora, Edward Lowassa, walipewa nafasi kubwa ya kuzungumza baada ya mgombea huyo kutopenya tano bora.
Kwa mujibu wa Kikwete, walizungumza yote na sababu ya kupata wagombea hao na sifa zao dhidi ya za wenzao na wakaafikiana na kupiga kura, ambapo Lowassa ambaye baadaye alitoka na kuhamia Chadema, alipiga kura.
Baada ya hapo walipatikana watatu, Magufuli, Balozi Amina na Dk Migiro ambapo katika Mkutano Mkuu, alipita Magufuli ambaye alisema ana kila sifa ya kuwa rais na kuongeza kuwa wananchi walisema yeye Kikwete ni mpole, hivyo baada ya kupata rais mpole, Tanzania inahitaji rais mkali.
Rais Kikwete alisema kampeni zinavyokwenda, anaona baada ya Uchaguzi Mkuu vyama vya upinzani vilivyojiunga katika mwavuli wa Ukawa, vitageuka jina na kuwa Ukiwa

Post a Comment

Previous Post Next Post