Meya Chadema aomba Rais Magufuli aungwe mkono

MEYA wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita (Chadema) amesema ni wakati wa kuweka itikadi za siasa pembeni na kumuunga mkono Rais John Magufuli katika jitihadi zake za kuijenga nchi.
Pamoja na hayo, mameya wa manispaa mbalimbali za jiji hilo, wamebainisha kuwa wamepanga kufanya kazi kwa ushirikiano kwa lengo moja la kulijenga jiji hilo na kuwaletea wananchi wake maendeleo bila kujali itikadi zao za kisiasa.
Akizungumza katika uzinduzi wa daraja la kisasa la Nyerere jijini Dar es Salaam juzi, Mwita alisema kwa sasa Tanzania inahitaji umoja na mshikamano. “Baada ya harakati za uchaguzi zilizomalizika mwaka jana, sasa uchaguzi umeisha ni kipindi cha kujenga taifa letu.
Tukienda kwa mtindo wa kugawana mbao hatutojenga taifa hili,” alisisitiza diwani huyo wa Vijibweni katika wilaya mpya ya Kigamboni. Alisema ni wakati wa kumsaidia Dk Magufuli kwa kuhamasisha watu wote wanaostahili kulipa kodi walipe kodi hiyo, ikiwa ni pamoja na kubuni vyanzo vipya vya mapato.
Alisema ili Dar es Salaam ipate maendeleo lazima wananchi hasa wafanyabiashara walipe kodi. “Tunahitaji kujenga madaraja, shule na hospitali. Msidhani Rais ana uwezo wa kutoa fedha mbinguni kwa ajili ya kujenga taifa hili. Lipeni kodi tupate maendeleo,” alisisitiza.
Kwa upande wake, Meya wa Temeke, Abdallah Chaurembo (CCM) alisema kwa sasa Jiji la Dar es Salaam lina mameya wanne na wote wamejipanga kufanya kazi kwa maslahi ya wana Dar es Salaam na kuheshimu viongozi wote.
“Usiwe na mashaka na kuhusu utekelezwaji wa Ilani ya CCM katika jiji hili, kwani hata bajeti ya halmashauri zetu zimetumia vigezo vilivyopo kwenye Ilani hiyo,” alisema Chaurembo akimueleza Rais Magufuli.
Akizindua daraja hilo, Magufuli ambaye amekuwa akisisitiza utaifa mbele badala ya mambo ya vyama, alisema, “Nafikiri kama Wizara ya Ujenzi itakubali kutokana na historia ya daraja hili, wapo viongozi wetu waliofanya makubwa, waliunganisha watu zaidi ya makabila 200, tukapendana bila kubaguana kwa vyama, rangi, lugha wala dini...Na daraja hili halitabagua mtu wa kupita, halitabagua CCM wala Chadema, wote hawa watapita.”

Post a Comment

Previous Post Next Post