Msanii ‘Roma Mkatoliki' na wenzake wapatikana

MSANII wa muziki wa hip hop, Ibrahim Mussa, ‘Roma Mkatoliki’ na wenzake watatu wamepatikana wakiwa wazima wa afya huku bado kukiwa na maswali mengi yanayohitaji majibu juu ya kutoweka kwao kwa takriban siku tatu.
Msanii huyo akiwa na wenzake, Monii Central Zone, Bin Laden pamoja na Imma ambaye ni msaidizi wa kazi katika studio za Tongwe Records walitekwa na watu wasiojulikana na kushikiliwa kwa siku tatu bila ya taarifa zozote.
Hali hiyo iliibua taharuki kwa wasanii na familia zao na hasa mke wa Roma aitwae Nancy ambae amekuwa akizunguka kwenye vituo kadhaa vya Polisi kumsaka mumewe. Jana taarifa za kuonekana kwa msanii huyo akiwa na wenzake hao zilipatikana takriban saa nane mchana ambapo walishikiliwa kwa zaidi ya saa tano katika kituo cha Polisi Oysterbay.
Gazeti hili lilitumia zaidi ya saa sita kumngoja msanii huyo na wenzake kwa lengo la kujua ni nini kiliwakuta lakini hata hivyo hawakupata nafasi ya kuzungumza nao kituoni hapo.
Saa moja usiku aliwasili wakili wao Peter Kibatala ambae aliingia moja kwa moja kituoni humo kuzungumza na wasanii hao. Baada ya takribani dakika 10 walitolewa wasanii hao bila ya kuonana na waandishi wa habari na wakapelekwa moja kwa moja katika Hospitali ya Mwananyamala kufanyiwa vipimo.
Licha ya vyombo mbalimbali vya habari ‘kupiga kambi’ kituoni hapo tangu mchana lakini Polisi walishindwa kuzungumzia hilo.

Post a Comment

Previous Post Next Post